ABUBAKAR SWIDDIIQ (ASSWIDIIQ)

NASABU  YA  SAYYIDINA  ABUBAKAR
Jina lake ni Abdullah bin Othman bin Amer bin Amru bin Kaab bin Saad bin Tayim bin Murrah bin Kaab bi Luay Al Kurashiy Al Taymiy, na uhusiano wake na Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) unakutana kwa Murrah bin Kaab, kwani jina la Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) ni Muhammad bin Abdillah bin Abdul Muttalib bin Hashim bin Abdu Manaf  bin Qusay bin Kilab bin Murrah bin Kaab.
Jina la baba yake ni Othman, lakini alikuwa maarufu kwa jina la Abu Quhafah, kwa hivyo Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akijulikana kwa jina Ibni Abi Quhafah, yaani mwana wa Abu Quhafah.
Mama yake ni Ummu l Khayr – Salma binti Sakhar bin Amer bin Kaab bin Saad bin Tayim bin Murrah bin Kaab na alikuwa binti ammi yake Abu Quhafah.


WAKE ZAKE NA WANAWE
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alioa wake wanne;
Wakati wa ujahilia (kabla ya kuja kwa Uislamu) alimuoa Qutailah binti Saad na akazaa naye Abdullah na Asmaa (Radhiya Llaahu ‘anhu).
Abdullahi aliingia katika Uislamu tokea siku za mwanzo na alifariki wakati wa ukhalifa wa baba yake.
Asmaa (Radhiya Llaahu ‘anhu) ni maarufu kwa jina la 'Dhaat nitwaqayn', na alipewa jina hilo baada ya kukata 'Nitaaq' mkanda wa kitambaa kinachofungiwa nguo kiunoni na kukifunika chombo kilichotiwa chakula alichokuwa akipelekewa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) pamoja na Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) walipokuwa pangoni wakati wa kuhajir kwenda Madina, na alikuwa mkubwa kwa umri kuliko Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha).
Aliolewa na Al Zubeir (Radhiya Llaahu ‘anhu) walipokuwa Makkah na alizaa naye watoto wengi mpaka alipomuacha akawa anaishi kwa mwanawe Abdullah bin Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyeuliwa Makkah.
Bibi Asmaa (Radhiya Llaahu ‘anha) aliishi miaka mia, na mwisho wa maisha yake alikuwa kipofu.

Wakati wa ujahilia Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alimuoa pia Umm Rumaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyezaa naye Abdul Rahman na Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) mke wa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na alifariki dunia wakati wa uhai wa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) aliyeteremka kaburini kwake siku ya maziko na kumuombea maghfira.
Abdul Rahman alipigana vita vya Badr na vita vya Uhud akiwa upande wa makafiri, na kabla ya kuanza vita vya Badr aliita kwa sauti kubwa akitaka mtu yeyote upande wa Waislamu aje kupambana naye na Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipotaka kutoka na kupambana na mwanawe huyo, Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alimzuwia na kumwambia;
"Tuache tukufaidi.".
Abdul Rahman alikuwa shujaa na mtupa mshale mwenye shabaha aliyesilimu baada ya mapatano ya Hudaibia (Sulhul Hudaibiah), akawa Muislamu mwema aliyepigana vita mbali mbali akiwa upande wa Waislamu, alishiriki katika vita vya Al Yamamah chini ya uongozi wa Khalid bin Waliyd (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakati majeshi ya Waislamu yalipopambana na majeshi ya Musailimah al Kadhaab (Mtume wa uongo), na yeye ndiye mkubwa wa watoto wa Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) na alifariki dunia ghafla mahali panapoitwa Hibsh karibu na mji wa Makka katika mwaka wa 53 H.


No comments:

Post a Comment